Site icon A24TV News

Mawakili wataka Sheria bora kulinda uhuru wa vyombo vya habari.

Mwandishi wetu,Dar es Salaam

Serikali imeshauriwa kufanya maboresho ya sheria za habari ili kuvipa uhuru vyombo vya habari na wadau wa habari kutekeleza vyema majukumu yao.

 

Baadhi ya sheria ambazo zinasimamia tasnia ya habari na uhuru wa kutoa maoni nchini, zimetajwa kuminya uhuru wa habari na uhuru wa kujieleza .

Sheria hizo pia zinatajwa kukinzana na Katiba ya Jamuhuri yha Muungano wa Tanzania, Ibara ya 18 na kifungu cha 19 cha Azimio la Umoja wa mataifa juu ya haki za binaadamu la mwaka 1948 vifungu ambayo vinazungumzia uhuru wa kutoa maoni na uhuru wa kutoa habari na kukusanya habari

Mhadhiri mwandamizi wa sheria wa chuo kikuu cha Tumaini- Makumira mkoani Arusha, Dk Elifuraha Lalkaita alisema kuna haja ya kufanyika maboresho ya sheria mbali mbali za habari nchini.

Dk Elifuraha alisema hivi sasa kutokana na sheria ya huduma za habari(MSA 2016) makosa mengi ya kitaaluma yamepewa adhabu kama makosa ya jinai jambo ambalo linaondoa uhuru kwa wanahabari na vyombo vya habari.

“nadhani yanahitajika maboresho haya makosa ya kimaadili yanapaswa kushughulia na vyombo vya kimaadili ama madai na ili kupunguza sura ya sheria kuwa na makosa mengi ya kijinai kwa wanahabari”alisema

Alisema pia sheria za habari zinapaswa kupunguza adhabu kali kwa ambao wanakosea ili kutoa uhuru wa wanahabari na wengine kufanyakazi na kutoa maoni yao bila hofu lakini pia kuvunja sheria.

Wakili Benedict Shebakaki akitoa mada juu ya haki ya faragha ulinzi wa matumizi taarifa za kielekroniki, katika mkutano wa watetezi wa haki za binaadamu wakiwepo wanahabari uliandaliwa na taasisi ya Defenddefenders alisema kunahitajika maboresho ya sheria.

Wakili Shebakaki alisema sheria kadhaa za habari ikiwepo sheria ya huduma za habari, sheria ya makosa ya mtandao , sheria ya mawasiliano ya kielekroniki na posta(EPOCA) na kanuni za maudhui ya mtandao zinamapungufu.

Shekakaki ambaye alikuwa wakili katika kesi ya Jamiii forums na kesi ya mchekeshaji Idris Sultani alisema kesi za wateja wake hao ambazo zilihusiana na masuala ya kusambaza habari zilitokana na changamoto za kisheria.

“Kuna baadhi ya vifungu katika sheria hizi vinaminya uhuru wa kujieleza na uhuru wa kitaaluma jambo ambalo linapaswa kuboreshwa”alisema

Alisema hata muswaada wa sheria mpya ya kulinda faragha ambao tayari umepitishwa na bunge bado una mapungufu ambayo yataposwa kuja kufanyiwa kazi ili kulinda uhuru wa kujieleza ,usiri na faragha za watu.

Wakili Onesmo ole Ngurumwa alisema kuna haja ya kuendelea n a mijadala ya maboresho ya sheria nyingi nchini, ili ziwe rafiki kwa wadau na hivyo kuchochea ukuaji wa sekta mbali mbali badala ya kuziathiri sekta hizo.

Serikali tayari imeanza mchakato wa maboresho ya sheria mbalimbali za habari ili kupunguza changamoto ambazo zinadaiwa kuathiri uhuru wa habari na kujieleza.

MWISHO