Site icon A24TV News

MIRADI MIWILI YA MAJI YENYE THAMANI YA ZAIDI YA MILIONI 740 YAKAMILIKA IKUNGI

 

Mkuu wa wilaya Mhe. Jerry C. Muro leo 09/01/2023 amefanya ziara ya mwisho ya ukaguzi wa miradi miwili ya maji ya kata za mtunduru na irisya jimbo la singida magharibi ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya uzinduzi wa miradi hiyo siku ya jumanne tarehe 10/01/2023 uzinduzi utakaofanywa na Mkuu wa mkoa wa singida Mhe. Peter Serukamba.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo Mhe. Muro amejiridhisha kuwa miradi imekamilika na wananchi wameanza kuyatumia maji safi na salama na kuwaomba wananchi wa kila eneo lenye mradi kujitokeza kwa wingi kesho.

Awali meneja wa Ruwasa wilaya ya Ikungi Mhandisi Hope Liundi amefafanua kuwa kila mradi umetengenezwa kulingana na mahitaji ya eneo husika ambapo amesema katika kata ya mtunduru mradi utanufaisha wananchi zaidi ya elfu tano mia nane na mradi utakuwa na uwezo wa kutoa zaidi ya lita laki moja na elfu kumi na saba kwa siku uku ukiwa na maeneo ya wazi ya kuchotea maji saba DP’s kwa kuanzia

Mhandisi Hope pia amesema mradi wa maji wa irisya utanufaisha wananchi zaidi ya elfu tatu na mia nane uku ukiwa na uwezo wa kuzalisha lita zaidi ya laki mbili na elfu arobaini kwa siku ambapo chanzo chake ni kisima kirefu na umechukua muda wa miezi sita kukamilika.

Mhe. Muro amehitimisha ziara yake kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia wilaya hiyo kupewa fedha zaidi ya bilioni 2 kwenye sekta ya maji ikungi na kuwahakikisha viongozi wa halmashauri za vijiji vyote viwili ambavyo ni wanufaika kuwa watafanya kila linalowezekana kuhakikisha mpaka mwaka 2025 wanafikia asilimia 85 ya upatikanaji wa maji kutoka asilimia 62 za sasa hivi

Mwisho