Site icon A24TV News

Waziri Kijaji Msipandishe Bei ya bidhaa wakati wa Mfungo wa Ramadhani na Kwaresma

Na Mwandishi wa A24TV Dar Es saalam

Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Mhe. Dkt Ashatu Kijaji (Mb.) amewaasa Wafanyabiashara kutokupandisha bei za bidhaa zote zinazotumika kwa wingi wakati wa Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na Kwaresma unaotarajiwa kuanza hivi karibuni.

Ameyasema hayo Februari 15, 2023 jijini Dar Es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa Habari kuhusu mwenendo wa bei za bidhaa muhimu nchini kwa mwezi Februari 2023.

Pamoja na hatua mbalimbali madhubuti zilizochukuliwa kuwa na bidhaa za kutosha za sukari na ngano, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kukabiliana na ongezeko la bei ya mchele kwa kutoa vibali sita (6) vya kuingiza mchele kutoka nje ya nchi ambapo hadi Machi, 2023 jumla ya tani 90,000 za mchele zinatarajiwa kuingia sokoni na hivyo kushusha bei ya bidhaa hiyo. Amesema Dkt. Kijaji.

Aidha Dkt. kijaji amewataka Wafanyabiashara nchini kuendelea kuzingatia misingi ya ushindani wa haki katika kufanya biashara na Wazalishaji wa bidhaa zote za viwandani kuongeza jitihada za kuzalisha bidhaa kwa ubora, viwango na ujazo unaohitajika sokoni ili kuunga mkono jitihada za Serikali za kukuza uchumi kwa manufaa ya Wananchi wote.

Vile vile ameitaka Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) kufanya ufuatiliaji wa karibu juu ya wafanyabiashara wanao zalisha bidhaa chini ya ujazo inaotakiwa ulioonyeshwa kwenye vifungashio na hatua madhubuti zichukuliwe kwa wote wataopatikana na kosa.

Aidha, Dkt Kijaji amesema bei za bidhaa za chakula, sabuni na vifaa vya ujenzi saruji, nondo bati Imeendelea kushuka na maguta ya kula imekuwa himilivu kutokana na kuimarika kwa uzalishaji wa ndani wa bidhaa hizo sambamba na usimamizi madhubuti wa mwenendo wa soko la bidhaa hizo uliofanywa na Wizara na taasisi zake.

Aidha amesema Mfumuko wa bei nchini Tanzania ni wa kiwango cha chini zaidi ikilinganishwa na nchi jirani ambapo kwa Tanzania kiwango cha mfumuko wa bei ni asilimia 4.9 kwa mwezi Januari 2023 ikilinganishwa na asilimia 9.1 ya Kiwango cha mfumuko wa bei nchini Kenya , asilimia 10.4 nchini Uganda na asilimia 21.7 nchini Rwanda kwa mwezi Januari, 2023.

Dkt.Kijaji pia amesema Wizara inaendelea kuratibu ukusanyaji wa takwimu za bei za mazao na bidhaa muhimu kama vile vyakula na vifaa vya ujenzi kutoka kwenye masoko yaliyopo katika Mikoa yote ya Tanzania Bara kupitia Wakusanya Taarifa za Masoko (Market Monitors) na Maafisa Biashara wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kulinda maslahi ya wadau wote ikiwa ni pamoja na wazalishaji, wafanyabiashara na watumiaji wa bidhaa husika.