Site icon A24TV News

MGOGORO WA KITALU B NGOMA NZITO MAJIBU YA RUFAA DANA DANA

Na Mwandishi wetu.

Sakata la mgogoro wa Mgodi wa Gem & Rock Venture uliopo Kitalu B katika Madini ya Tanzanite Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara limeingia sura Mpya baada ya Kamishina wa Madini Nchini,Dkt Ibraharman Mwanga kusema kuwa rufaa ya kupinga kufungiwa kwa Mgodi huo amemtumia Mkurugenzi wa Mgodi  huo Joel Mollel maarufu kwa jina la Saitoti  wakati Saitoti anasema hana taarifa yoyote juu ya Maamuzi ya rufaa yake.

Mnamo Machi 13 mwaka huu wachimbaji wa Mgodi wa Gem & Rock Venture Uliopo Kitalu B Wakiongozwa na Saitoti walivamia mgodi wa kitalu C zaidi ya mita 650 kinyume na utaratibu na kufanya uzalishaji wa madini ya zaidi ya kilo 4  na kuwashambulia viongozi wa Taasisi za ulinzi za serikali na serikali iliamua kuufunga mgodi huo baada ya taarifa rasmi ya kitaalamu kubaini kuwa Saitoti na wafanyakazi wake walichimba madini ndani ya Kitalu C.

Taarifa hiyo ya uchunguzi ilitolewa Machi 28 mwaka huu , 2023 na Afisa Mfawidhi wa Madini Mirerani, Mernadi Msengi mbele ya Waandishi wa habari lakini Saitoti hakukubaliana na Maamuzi hayo na kukata rufaa kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini kupiga Maamuzi hayo kwani alidai hakuingia katika Mgodi wa Kitalu C kuchimba kinyemela Madini hayo na pia aliomba kurudishiwa Madini yake kilo 4 yaliyotaifishwa na serikali.

Kufuatia hatua hiyo ya kusimamishwa kwa shughuli za uzalishaji katika Mgodi wa Kitalu B ndipo Mmiliki wa mgodi huo aliamua kukata rufaa ya kutoridhishwa na maamuzi ya wizara juu ya kuyashikilia madini hayo na .

Wakati Kamishina anasema maamuzi ya Rufaa yameshatumwa kwa Mkurugenzi wa Gem & Rock Venture,Joel Mollel Maarufu kwa jina Saitoti na hawezi kuyaongelea kwenye Vyombo vya Habari,Saitoti analalamika kuwa hana majibu ya rufaa yake na Mgodi wake umefungwa zaidi ya miezi miwili na anaingia gharama kubwa kuwalisha wafanyakazi wakati watendaji wa serikali wamekalia rufaa yake.

” Mimi Sina taarifa ya Rufaa yangu hadi Sasa na Kama Kamishina anadai Ametuma,Ametuma kwa njia ipi ? Akueleze ninachojua mie Nasubiri rufaa yangu màana nimeenda hata kwa Afisa Madini Mirerani kuuliza Hana majibu Sasa hayo majibu ya rufaa amemtumia Nani na lini” alisema Saitoti

Kamishina alipoulizwa tena juu ya Saitoti kusema kuwa hana taarifa ya majibu ya rufaa,Alisema kimsingi yeye ndiyo aliye kata rufaa na tumeshamjibu, sasa nyie mkisema niwambie ni kitu gani kiliamuliwa katika rufaa hiyo alisema haiwezekani na kutoa Maelekezo kuwa atafutwe Saitoti kwani ndio Mwenye wajibu wa kueleza majibu ya rufaa yamekuwaje ameshinda au ameshindwa na sio Wizara ya Madini.

Alipotafutwa Afisa Madini Mfawidhi Mirerani,Mernad Msengi yeye alisema kuwa Wenye Mamlaka ya kujua Maamuzi ya rufaa ni viongozi wake wa juu kwani rufaa ilikatwa kwa Katibu Mkuu Wizara ya Madini hivyo wao wana Mamlaka ya kuizungumzia rufaa hiyo.

Mwisho