Site icon A24TV News

DKT. YONAZI APONGEZA HATUA ZA UJENZI WA ENEO LA MNARA WA MASHUJAA.

Na Doreen Aloyce ,Dodoma

KATIBU MKUU Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi amepongeza maendeleo ya ujenzi wa Uwanja wa Mashujaa unaojengwa katika Mji wa Serikali, Mtumba Jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi (kulia) akiwa na Mratibu wa Kamati ya zoezi la Serikali kuhamia Dodoma Bw. Meshack Bandawe wakikagua Eneo la mradi wa Ujenzi wa Mnara wa Mashujaa Mtumba Dodoma.

Dkt. Yonazi ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea na kukagua ujenzi huo ambapo ameeleza kwamba unaendelea vizuri na unatarajiwa kukamilika mapema kabla ya Julai 25 mwaka huu ili uweze kutumika kwa ajili ya shughuli za Mashujaa.

Ameongeza kuwa mpaka sasa hatua iliyofikiwa ni ujazaji wa udongo na kushindiliwa huku akimsisitiza mkandarasi kuhakikisha ujenzi unafanyika kwa kuzingatia ubora na uimara wa miundombinu ndani ya muda uliopangwa.

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi akikagua Ramani ya Mfumo wa Maji Taka katika Mji wa Serikali Mtumba wakati wa ziara yake aliyoifanya ya kutembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Mnara wa Mashujaa Jijini Dodoma.

“Kazi inaendelea vizuri kwa ajili ya ujenzi wa Uwanja wa Mashujaa maeneo mbalimbali yameshajazwa udongo na kushindiliwa hivyo tunaamini mkandarasi wetu SUMA JKT atafanya kazi nzuri,” Amesema Dkt. Yonazi.

Aidha kuhusu mfumo wa maji taka amebainisha kuwa itajengwa katika hali ya bora ili kuhakikisha Mji wa Serikali unakuwa katika mandhari nzuri na ya kuvutia kulingana na malengo ya Serikali ya kukamilisha Mji wa Serikali.

Mhandisi Evance Antony kutoka SUMA JKT akitoa maelezo kuhusu maendeleo ya Ujenzi wa Mnara wa Mashujaa.

= MWISHO=