Site icon A24TV News

JAMII YAASWA KUZINGATIA MAADILI

Na Pamela Mollel,Arusha

Jamii imeaswa kuzingatia maadili na kuacha vitendo viovu na kufanya yale yanayo mpendeza Mungu ikiwemo kufanya kazi kwa bidii na uaminifu katika nafasi tunazopewa ili nchi iweze kuwa na maendeleo na kupiga hatua kiuchumi.

Hayo yameelezwa na Baba Askofu Dkt. Solomoni Jacob Massangwa ambae pia ni Mkuu wa Dayosisi ya kaskazini kati kanisa la kilutheri Tanzania katika ibada ya kumstaafisha parishworker wa jimbo la Arusha Mashariki Bi. Rebeca Christopher Mungure ambae amekuwa kwenye utumishi takribani miaka 40.

Askofu Dkt. Solomoni Masangwa alisema kuwa jamii kwa ujumla inapaswa kuiga mfano mzuri kutoka kwa Parishworker huyo aliyejitoa kumtumikia Mungu tendo ambalo limempendeza Mungu na wanadamu.

“Viongozi na watumishi katika Taifa letu la Tanzania ni vizuri kuiga mfano wa Bi.Rebeca kwa kufanya kazi kwa bidii,maarifa na uaminifu pamoja na uvumilivu mkubwa na mwisho wao utakuwa baraka kwao na kwa Taifa letu”alisema Baba Askofu.

Kwa upande wake Bi. Rebeca baada ya kustaafu kwa heshima akatoa shukrani zake kwa Dayosisi na Kanisa huku akipanda mti kama alama ya kumbukumbu katika usharika wa Kimandolu

“Namshkuru Mungu sanaaa kwa tukio kubwa la leo la kustaafu kwangu kwa heshima nawashukuru sanaaa Dayosisi na kanisa wakiongozwa na Mkuu wa jimbo letu la Arusha Mashariki Mch.Daniel Mahawe kwa kuwa mstari wa mbele kwa jambo hili”alisema Bi.Rebeca.

Aidha aliwashukuru wote waliojitoa kwa zawadi mbalimbali zikiwemo fedha na gari alilozawadiwa na idara ya wanawake.

Naye Mwenyekiti idara ya wanawake jimbo la Arusha mashariki Bi. Nembrisi Samwel akaeleza utumishi wa mfano aliokuwa nao bi. Rebeka hivyo wakina mama wamemwaga kwa kumzawadia gari yenye thamani ya sh. Milioni 14 na kueleza kuwa huu uwe mfano kwa jamii katika utumishi wa uaminifu.

 

Mwisho.