Site icon A24TV News

LATRA YAMALIZA MGOMO WA DALADALA JIJINI ARUSHA! BAJAJI KUONDOLEWA KATIKATI YA MJI

Na Geofrey Stephen Arusha .

Baada ya kuonja joto la kukosekana kwa usafiri kwa siku ya jana  kwa mgomo wa Dala Dala kwa siku nzima Jijini Arusha Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (Latra)Mkoa wa Arusha imetangaza kumaliza mgomo kwa madereva wa daladala uliodumu kwa siku moja baada ya kukubaliana na viongozi wa daladala jijini Arusha na kuahidi kutatua changamoto za bajaji zinazolalamikiwa kufanyakazi kinyume cha sheria za usafirishaji

Akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake, ofisa mwandamizi wa LATRA mkoani Arusha , Amani Mwakalebela alisema ofisi yake imeahidi hadi tarehe 10 mwezi huu kushughulikia kero za daladala zinazotokana na bajaji kufanya kazi za daladala kinyume na utaratibu.

Aidha Mwakalebela aliahidi kuchukua hatua kali kwa bajaji zisizo na usajili ikiwemo kuziondoa barabarani bila kujali baadhi ya bajaji zinazotajwa kumilikiwa na vigogo hapa Arusha.

 

“Kuanzia sasa hatuta kuwa na mzaha tena tutazikamata na kuziondoa barabarani Bajaj zote zisizo na usajili, jiji la Arusha limejaa wazipeleke wilaya zingine”

“Hivi sasa Ruti za daladala zilizokufa sababu ya Bajaji ni pamoja na Ruti ya kutoka mjini kwenda Sanawari ya Juu ,Majengo juu,Ngusero ,Engosheratoni,Kijenge juu,Kisongo na Lemara”

“Tulitegemea Bajaji wanafanya biashara ya kukodishwa kama leseni yao inavyosema, lakini wanafanyakazi kama daladala ni lazima tuziondoe barabarani kwa kufanya uhakiki wa kina kupitia ofisi ya LATRA na baada ya uhakiki tutazipa namba ubavuni na kupangia vituo na watakaoenda kinyume tutazikamata na kuziweka kwenye yadi ya serikali na hazitatoka”

 

Alisema katika jiji la Arusha bajaji zenye usajili ni 350 tu lakini hadi sasa kuna bajaj zaidi ya 2000 zinafanyakazi kinyume na utaratibu kwa kuwa Bajaji zinasajiliwa kama pikipiki ya miguu mitatu ambayo itafanyakazi kwa kukodishwa na sio kukusanya abiria.

Naye mwenyekiti wa daladala mkoa wa Arusha,Billy Matemwe alisema wamekubaliana na LATRA kuruhusu daladala zirejee barabarani hadi tar 10 mwezi huu wakati wakifanyiakazi madai ya madereva wa daladala.

Mwisho .