Site icon A24TV News

TASAC kutengewa bilioni 83.1 ujenzi wa Bandari Bahari kuu na maziwa makuu.

Na Doreen Aloyce, Dodoma

Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limesema Serikali imetenga kiasi cha fedha shiling bilioni 83.1 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya ujenzi wa Bandari katika bahari kuu na maziwa makuu hapa nchini kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Pia limesema limejipanga kununua boti tatu za uokozi katika Ziwa Victoria ambazo zitakwenda kusaidia kutatua changamoto ambazo zimekuwa zikijitokeza pindi ajali zinapotokea.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Shirika Hilo, Kaimu Abdi Mkeyenge wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya TASAC na mwelekeo wake katika mwaka wa fedha 2023/2024 katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo jijini Dodoma.

Amesema katika boti hizo tatu zitakazonunuliwa mbili zitakuwa ni za mwendonkasi kwaajili ya ukokozi na Moja itakuwa kwaajili ya kubebea majeruhi na wagonjwa (Ambulance) .

“Boti hizi tatu zitatumika kufanya uokozi katika ajali ambazo zimekuwa zikitokea katika Ziwa Victoria ambapo mbili zitakuwa ni za meendo kasi na Moja itatumika kama ambulance kwa ajili ya majeruhi”amesema

Aidha amesema TASAC imeendelea kuimarisha udhibiti huduma za usafiri majini, na kuhakikisha kuna ushindani sawia miongoni mwa watoa huduma.

Aidha limesema kuwa linafanya ufuatiliaji, tathmini na kutoa maelekezo kuhusu utekelezaji wa vigezo na viwango vya ubora wa huduma (performance standards and Benchmarks) kwa watoa huduma za bandari na usafiri majini.

“Tunaendelea kuratibu maombi ya tozo za usafiri wa meli katika Maziwa (Victoria na Nyasa) na kuhakikisha viwango vya tozo vinavyotumika haviathiri ushindani wa kibiashara;

“Lakini pia zoezi la urasimishaji wa bandari bubu Tanzania bara ambapo bandari bubu kumi na tatu (13) zilizowasilishwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA) kwa ajili ya urasimishaji zilikaguliwa na kufanyiwa tathmini ya kina kwa kushirikiana na TPA, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Baraza la Usimamizi wa Mazingira (NEMC)”amesema Mkeyenge

Kadhalika amesema bandari bubu kumi zilionekana kukidhi vigezo hivyo na kupendekezwa kwa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi) (WUU-U) kwa ajili ya kurasimishwa kwa mujibu wa sheria

“waendeshaji wa zilizokuwa bandari bubu binafsi tano (05) za Mwanza ambazo ni miongoni mwa zilizokuwa bandari bubu ishirini (20) zilizorasimishwa kupitia Tangazo la Serikali (GN) namba 293/2022 wamepewa leseni za uendeshaji huku TPA wakielekezwa kusimamia kwa karibu bandari kumi na tano (15) zilizobakia.

Akizungumzia kuhusu Kuboresha usalama, ulinzi kwa usafiri majini na kudhibiti uchafuzi wa mazingira baharini utokanao na meli amesema Shirika limetimiza lengo hilo la kimkakati kwa kuendelea kusimamia usalama wa vyombo vya usafiri majini kwa
Kufanya ukaguzi wa meli kubwa na vyombo vidogo vya majini.

“Shirika lilifanya kaguzi za usalama kwa meli kubwa zibebazo tani 50 au zaidi ili kuhakikisha kuwa ni salama na zinaendeshwa na mabaharia wenye sifa katika mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, Tanga, Mwanza, Kagera, Kigoma na Mbeya ambapo katika kipindi cha Julai, 2022 hadi Juni, 2023, Shirika lilifanya jumla ya kaguzi za meli kubwa 288 ambapo kaguzi 165 zilikuwa za meli za kigeni na kaguzi 123 zilikuwa meli za ndani.”amesema

Kuhusu uratibu Shughuli za Utafutaji na Uokoaji Majini amesema Kituo cha Utafutaji na Uokoaji Majini kilichopo Dar es Salaam kinachoratibiwa na TASAC kiliendelea kufanya shughuli zake katika kipindi cha Julai, 2022 hadi Juni, 2023 ambapo kituo kilipokea taarifa 4 za ajali zilizohusisha vyombo vya majini ambazo zilitokea katika eneo la maji ya Tanzania.

Katika ajali hizo jumla ya watu 61 walihusika ambapo watu 58 sawa na 95% waliokolewa na watu 3 sawa na 5% walipoteza maisha.

Nae Mkurugenzi wa Idara ya Habari -Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa amesema Serikali inataka kushirikiana na sekta binafsi kuendesha Bandari, mikataba na watakaoendesha bado haijasainiwa.

“Sasa hivi ndio wataalamu wako mezani kuzungumza kuhusu mikataba, muda na gharama lakini hakuna bandari iliyouzwa, wataalamu watakapokamilisha majadiliano tutaangalia maslahi yetu yako wapi na maoni yanayotolewa na Watanzania yatazingatia Serikali iko macho wakati wote kuhakikisha maslahi ya Watanzania yanalindwa”amesema Msigwa

Mwisho