Site icon A24TV News

WANANDOA MALIZENI MIGOGORO KUKOMESHA WIMBI LA WATOTO MITAANI.

Na Richard Mrusha

AFISA ustawi wa jamii manispaa ya Ubungo jijini Dar Naamini Nguve, amewataka wanandoa nchini wajitahidi kumaliza migogoro yao ili kupunguza wimbi la watoto wa mitaani.

Nguve amesema kuwa katika kituo cha mabasi maarufu Magufuli kilichopo manispaa ya Ubungo jijini hapa wamekuwa wakipokea makundi ya watoto chini ya miaka 18, vijana, wazee pamoja na walemavu kutoka katika Mikoa mbalimbali hapa nchini kwa lengo la kuja kusaka ajira.

Afisa Ustawi wa jamii manispaa ya Ubungo, Nguve, akizungumza na waandishi wa Habari Ofisini kwake.

Afisa huyo wa ustawi wa jamii amesema kuwa hatua hiyo wamebaini baada ya watoto hao kufika jijini Dar na kukosa ajira na wanapohojiwa chanzo ni migogoro ya ndoa na wengine wameletwa ili kutumikishwa lakini wanapofika jijini hapa waliowaita wanazima simu na hivyo kuomba msaada wa kurejeshwa walikotoka

Nguve ambaye ni Afisa Ustawi wa Jamii manispaa ya Ubungo Jijini hapa aliyasema hayo Jualai 27,2023 alipokuwa akizungumza na waandishi wa Habari walitembelea kituo cha mabasi maarufu Magufuli kilichopo manispaa ya Ubungo jijini Dar kwa lengo la kuangalia maendeleo ya kituo hicho ndipo ikaibuka hoja hiyo.

“Hapa kituo cha Mabasi Magufuli tumekuwa tukipokea makundi ya vijana, watoto chini ya umri wa miaka 18 wakiwemo wazee vikongwe na walemavu kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini kuja kutafuta kazi, wengine wanakuja kwa kupigiwa simu lakini wakifika Dar simu zinazimwa”alisema Nguve na kuongeza.

“Wakisha zimiwa simu ndipo wanashauriwa na baadhi ya watu kuwa waje hapa kwa lengo la kuomba msaada wa kurejeshwa kwao, ambapo na sisi kwakushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo wasafirishaji pamoja na wahisani kupitia asasi za kiraia tunawasiliana na ndugu au familia zao uko waliko toka tukijirisha tunawasafirisha,”
Alisema Afisa ustawi wa jamii.

Aliongeza kuwa katika katika mahojiano yao kabla ya kuwarejeshea nyumbani kwao walibaini chanzo ni migogoro ya ndoa, na kuhusu wazee walemavu alisema kuwa wengi wanaletwa na kupangishiwa vyumba vya bei nafuu na kupewa baiskeli za mikokoteni ili kuingia mitaani na kufanya kazi ya ombaomba.

Kutokana na hali hiyo afisa ustawi wa jamii huyo alitumia nafasi ya ujio wa wanahabari hao katika kituo cha mabasi kuwataka watoto, vijana na watu wengine wanaoitwa kuja jijini Dar kwa lengo la kupewa kazi wasije na nauri ya kutoka huko walikotoka bali wahakikishe wanakuja na nauri ya kurudia iwapo waliowaita wamejificha kwa kuzima simu

Hata hivyo meneja wa kituo hicho Isaka Waziri ameipongeza serikali kupitia halmashauri ya manispaa ya Ubungo kubuni chanzo kingine cha ukusanyaji wa mapato ya kiingilio getini kwa kutumia mfumo kidigitali N KAD ambacho kimekuwa na tija baada ya mapato kuongezea kutoka kiasi cha shilingi Milioni 3.4 mpaka kiasi cha shilingi Milioni 6.5.

Pia meneja huyo akizungumzia hali ya ulinzi wa mali za wateja katika kituo hicho alisema kuwa kituo kinazingatia sana suala la usalama ikiwemo kudhibiti uharifu ambapo alisema kubwa mpaka wakati anazungumza na wanahabari tayari walikuwa wamekamatwa wapiga debe wasio waaminifu zaidi ya 40.

“Naahidi zoezi hili la kukamata waharifu litakuwa ni endelevu ndiyo maana ofisi hiyo kwa kushirikiana na serikali pamoja na wamiliki wa mabasi tunajitahidi kurejesha makwao watoto ambao wanaingia kwa njia haramu hapa jijini na wale wanaoletwa kutumikishwa na baadae kuwakosa watu wao huo ni wasije kubwa vibaka kama hawa wapiga debe,”alisema Waziri meneja wa kituo cha mabasi Magufuli
Mwisho.