Site icon A24TV News

MADINI, UFARANSA ZAJADILI KUSHIRIKIANA

Na mwandishi wetu Dodoma

Viongozi na Watendaji wa Wizara ya Madini na Taasisi za Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) na Tume ya Madini leo Februari 15, 2024. wamekutana na ugeni wa Kidplomasia kutoka Ubalozi wa Ufaransa nchini na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti ya Ufaransa (BRGM).

Lengo la ugeni huo lilikuwa ni kutambua fursa za uwekezaji hususan kwenye madini muhimu na mkakati na kuangalia maeneo ya ushirikiano katika Sekta ya Madini nchini.

Katika kikao hicho kilichongozwa na Naibu Katibu Mkuu Msafari Mbibo, Mtendaji Mkuu wa GST Dkt. Mussa Budeba amebainisha maeneo muhimu ya ushirikiano kuwa ni pamoja na uwekezaji katika shughuli za utafiti wa kina wa madini na kuwajengea uwezo wanasayansi katika maeneo mbalimbali ya jiosayansi.

Masuala mengine yaliyogusiwa ni pamoja na kuwajengea uwezo wanajiosayansi kwenye masuala yanayohusu majanga ya asili ikichukuliwa mfano wa tukio la hivi karibuni lililotokea Wilayani Hanang la kumomonyoka kwa udongo na masuala yanayohusu akili bandia.

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu Mbibo ameueleza ujumbe huo kuwa bado ipo nafasi ya kukutana na kuendeleza ushirikiano baina yao na GST katika maeneo yaliyokubalika.

Mwisho.