Site icon A24TV News

MBUNGE APENDEKEZA WABAKAJI WAKATWE UUME!

By A24 Tv

Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Mkoa wa Iringa Ritta Kabati amependekeza kutolewa uume kwa wanaume wanaotiwa hatiani kwa kisa la ubakaji ili kudhibiti vitendo hivyo baada ya hivi karibuni kuibuka na kukithiri Kwa vitendo hivyo nchini.

Kabati amependekeza hilo bungeni jijini Dodoma wakati akiuliza swali la nyongeza Kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

“hili tatizo limekuwa kubwa sana hapa nchini, mi naona je! Kuna uwezekano labda watolewe uume maana yake imekuwa ndio tatizo kubwa sana”

Akijibu swali hilo kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Jumanne Sagini amekiri kuwa jambo hilo linaudhi huku akieleza kuwa suala la kukatwa uume halipo kwenye sheria za nchi.

“Kama tutafika hatua hiyo ni pale ambapo Bunge lako litakuwa limerekebisha Sheria na kuruhusu hicho anachokisema Mheshimiwa Mbunge.” Jumanne Sagini

Kwa upande wa Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Jumanne Sagini ametaja adhabu mbalimbali ambazo kwa mujibu wa sheria ya makosa ya adhabu zinatolewa kwa mtu aliyetenda makosa ya ubakaji.

Amesema kifungu cha 131 kifungu kidogo cha 1 cha sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16 kimeainisha adhabu ya makosa ya kubaka kuwa ni kifungo kisichopungua miaka 30, viboko, na mahakama inaweza kutoa amri ya kumlipa fidia muathirika wa tukio.

Aidha, amesema kuwa kifungu cha 131 kifungu kidogo cha 3 cha sheria hiyo kimeainisha kuwa ikiwa muathirika wa tukio ni mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 10 adhabu pekee iliyopo ni kifungo cha maisha jela.