Site icon A24TV News

SERIKALI KUFANYA SENSA YA UZALISHAJI WA VIWANDA KUFANYIKA BARA NA VISIWANI

Na Doreen Aloyce,Dodoma

SERIKALI ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania inatarajia kufanya Sensa ya uzalishaji Viwandani kwa mwaka wa Rejea 2023(Census of Industrial Production 2023) mwezi machi 2025.

Hayo yamesemwa jijini na Waziri wa Viwanda na Biashara,Dkt.Selemani Jafo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa takwimu kuhusu sensa ya uzalishaji Viwandani kwa mwaka wa Rejea 2023 kufanyika mwezi machi 2025.

Aidha amesema Sensa ya uzalishaji Viwandani ya mwaka wa Rejea 2023 itakuwa ya kwanza kufanyika katika pande zote mbili za muungano wa jamuhuri ya Tanzania tangu mwaka 1964.

Dkt.Jafo ameeleza kuwa suala la takwimu ni miongoni mwa mambo ya muungano (namba 20 kwenye orodha ya mambo ya muungano) ya katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977,Tanzania bara ilifanya Sensa za uzalishaji Viwandani mwaka 1963,1978,1989 na 2013 na Kwa upande wa Zanzibar zilifanyika mwaka 1989,2002,2008 na 2012.

“Lengo la Uzalishaji Viwandani ya mwaka wa Rejea 2023 ni kupata taarifa za kina za kitakwimu zitazowezesha Serikali na wadau kufanya maamuzi yenye ushahidi wa kitakwimu katika kuhuisha na kuboresha Sera,mipango na programu za maendeleo ya Sekta ya viwanda na uchumi wa Kitaifa Kwa ujumla,”alisema Dkt.Jafo.

Aidha ameongeza kuwa matokeo hayo yatatumika kupima utekelezaji wa mpango wa taifa wa maendeleo wa miaka mitano(FYDP 111),programu za kikanda kama vile dira ya Afrika mashariki 2050,Agenda ya maendeleo ya Afrika 2063 na malengo endelevu ya Dunia 2030( SDGs) hususani lengo namba 6 kuhusu upatikanaji wa maji safi na salama,lengo namba 7 kuhusu upatikanaji wa nishati safi na gharama nafuu na lengo namba 9 kuhusu maendeleo ya viwanda,ubunufu na miundombinu.

Vilevile taarifa za viwanda zitakazokusanywa zitahusisha shughuli za kiuchumi zilizofanyika katika viwanda ambapo shughuli zitakazojumuishwa ni pamoja na utengenezaji wa bidhaa zae viwanda,uchimbaji wa madini na kokoto, uzalishaji na usambazaji wa umeme,gesi,mvuke na kubadilisha hali joto au baridi na usambazaji wa maji safi,mifumo ya kukusanya maji taka,udhibiti wa taka na shughuli za urejeshaji(recycling).

Pia amesema Sensa ya uzalishaji Viwandani ya mwaka 2023 itakusanya taarifa kutoka viwanda vyote ambavyo vimegawanywa katika makundi mawili makuu ambapo Kuna kundi la viwanda vyenye wafanyakazi kuanzia kumi au zaidi na kundi la viwanda vyenye wafanyakazi kuanzia mmoja hadi tisa.

Na kwa baadhi ya shughuli za kiuchumi kwa viwanda vidogo amesema zitafanyika Kwa sampuli kutokana na wingi wa viwanda na sifa zinazofanana.

Kwa upande wake Mtakwimu Mkuu wa Serikali Dkt.Albina Chuwa amesema kuwa Sensa hiyo ya uzalishaji viwanda itafanyika kwa miezi tatu,yaani Mwezi Machi,Aprili na Mei ambapo Mwezi Juni wanatoa matokeo na kuelezea wananchi mafanikio makubwa ndani ya Sekta ya Viwanda ambayo inachukua taswira kubwa katika nchi yetu.

Mwisho